Wednesday, September 25, 2024

UFUGAJI WA MENDE FURSA MPYA INAYOCHANGIA UCHUMI

 

 

UFUGAJI WA MENDE: 

FURSA MPYA INAYOCHANGIA UCHUMI

Ufugaji wa mende ni sekta inayokua kwa kasi hapa nchini kutokana na faida zinazopatikana kutoka kwa wadudu hawa. Kasi hii imechochewa na uelewa unaoendelea kuongezeka juu ya thamani ya mende katika masuala mbalimbali kama chakula, lishe ya mifugo, na hata uzalishaji wa bidhaa za urembo. Ufugaji wa mende hauhitaji masharti mengi wala gharama kubwa, jambo linalowavutia wafugaji wengi kujiingiza katika biashara hii.

Kuna zaidi ya aina 400 za mende duniani, lakini aina 30 pekee hupatikana katika makazi ya binadamu. Kati ya hizi, aina 4 zinajulikana kuwa kero katika nyumba. Hata hivyo, mende wanaofugwa kwa ajili ya chakula cha mifugo, binadamu, na kutengeneza bidhaa za urembo ni wale waliofanyiwa mseto wa kisayansi kwa kuchanganya mende wa Asia, Ujerumani, na Marekani. Kwa kitaalamu, aina bora zaidi ya mende huyu anajulikana kama Diploptera punctata.

Periplaneta Americana  (American Cockroach) aina hii ya mende ni maarufu inayofugwa kwa ajili ya protini na utengenezaji wa dawa. Mende hawa wanakua haraka na ni hodari wa kustahimili mazingira magumu, asili y amende hawa  ni Afrika, lakini wameenea duniani kote. Hupatikana sana katika maeneo ya tropiki na hali ya joto. Sifa ya mende hawa  ni wakubwa kuliko aina nyingine nyingi, na wana urefu wa hadi sentimita 5. Wana uwezo wa kuruka, na wanapendelea mazingira yenye unyevunyevu kama vile jikoni, mabomba ya maji, na vyooni.

Aina nyingine ni Mende wa Ujerumani (German Cockroach) na jina la kisayansi wanajulikana kama Blattella germanica, asili ya mende hawa  ni Asia, lakini wameenea kote duniani, hasa katika maeneo ya mijini na sifa kubwa ya mende hawa ni  ni mende wadogo wenye urefu wa takriban sentimita 1.5. Wanajulikana kuwa na uwezo wa kuzaa kwa haraka sana na wanapendelea maeneo yenye joto, hasa jikoni na vyooni.

Wako wengine wanaojulikana Asia (Asian Cockroach) na jina la kitaalamu wanajulikana kama Blattella asahinai na hawa asili yao ni Asia ya Kusini-Mashariki, lakini wameenea katika maeneo mbalimbali duniani, hususan Amerika Kaskazini, sifa yao kubwa  hufanana sana na mende wa Ujerumani lakini wana uwezo mzuri zaidi wa kuruka. Wanapenda maeneo yenye mwanga kama bustani na nje ya nyumba, tofauti na mende wengine wanaopendelea giza. Wengine ni Mende wa Smoky Brown (Smokybrown Cockroach) jina la Kisayansi Periplaneta fuliginosa, Mende wa Brown Banded (Supella longipalpa na aina nyingine nyingi ambayo


FAIDA ZA UFUGAJI WA MENDE

Ziko faida nyingi za ufugaji wa mende lakini faida hizi tunaweza kuziweka katika makundi makubwa mawili ambapo ni faida za kiuchumi na Kiafya

KIUCHUMI :

Mende hufugwa kwa gharama ndogo na kuuzwa kwa bei nzuri, hususan kama chakula cha wanyama kama samaki na kuku. Pia, biashara ya mende inatoa fursa kwa kupunguza taka za chakula, kwani mende wanaweza kula mabaki ya vyakula na taka nyingine za kikaboni.

Uuzaji wa mende waliofyekwa na kukaushwa unaweza kufikia hadi dola 20 kwa kilo moja, na hivyo kutoa faida kubwa kwa wafugaji.

KIAFYA :

Chakula cha Binadamu: Nchini Tanzania na duniani kote, baadhi ya watu hutumia mende kama chakula. Hasa katika nchi kama Denmark, Brazil, na China, soko la mende kwa ajili ya chakula ni kubwa.

Lishe ya Mifugo: Mende ni chanzo kizuri cha protini kwa mifugo, hasa kuku. Utafiti umeonyesha kuwa mende wana kiwango kikubwa cha protini ukilinganisha na vyakula vingine, hivyo wafugaji wengi hupendelea kuwapa mende badala ya dagaa.

Taaluma: Katika masomo ya biolojia, mende hutumika sana kwenye majaribio ya kisayansi. Hii inatoa fursa kwa wafugaji kuwauza mende kwa shule na taasisi za elimu kwa ajili ya majaribio.

UZALISHAJI NA UTAGAJI

Kwa kawaida, mende huchukua takriban miezi miwili na nusu kufikia umri wa kuvunwa, endapo watapatiwa chakula na maji ya kutosha. Mende wana uwezo wa kuishi hadi miaka minne, na kila mmoja ana uwezo wa kutaga kati ya mayai 55 hadi 70 mara tatu kwa mwaka. Endapo watapatiwa mazingira rafiki, asilimia kubwa ya mayai hayo hutatua na kuzalisha mende wachanga.

UJENZI WA BANDA

Banda la kufugia mende linaweza kujengwa kwa ukubwa na muundo tofauti, kulingana na mtaji na malengo ya mfugaji. Kwa wale wanaofuga mende kwa ajili ya chakula cha binadamu, inashauriwa kuwa na mazingira safi na mazuri zaidi kuliko wale wanaofuga kwa ajili ya chakula cha mifugo. Zingatia yafuatayo wakati wa kuandaa banda:

Tengeneza mazingira yenye giza kwani mende hawapendi mwanga.

Hakikisha banda haliingii maji wala mwanga mwingi.

Tumia masanduku maalumu ya mbao yenye uwezo wa kuhifadhi mende bila kuruhusu watoke nje.

CHAKULA

Mende hula aina mbalimbali za chakula ambazo hazigharimu sana. Chakula cha mende ni rahisi na kinapatikana kwa wingi nchini, ikiwa ni pamoja na:

Unga wa mahindi na muhogo,

Viazi mviringo (vilivyo bora au vilivyoharibika),

Matunda na mboga,

Maharage yaliyopikwa na kupondwa.

Kwa kawaida, mende wanapopewa chakula cha vizuri, baada ya wiki mbili wanakuwa tayari kuvunwa wakiwa na uzito wa gramu 5, ambao ni uzito bora kwa matumizi mbalimbali.

SOKO LA MENDE

Soko la mende linaendelea kuimarika kutokana na uelewa unaoongezeka juu ya faida za wadudu hawa. Kuna masoko kadhaa:

1. Chakula cha Binadamu: Wateja wakuu ni wachina na watu wengine wa nje ya nchi.

2. Chakula cha Mifugo: Wafugaji wa kuku hutumia mende kama mbadala wa dagaa.

3. Taaluma: Shule na taasisi za elimu hununua mende kwa ajili ya majaribio ya kisayansi.

4. Wafugaji Wapya: Wafugaji wapya wanahitaji mbegu za mende kwa ajili ya kuanzisha biashara zao, hivyo kuna fursa kubwa ya kuuza mende kama mbegu.

MADHARA YA MENDE

Ingawa ufugaji wa mende una faida nyingi, kuna madhara ambayo hujitokeza wanapokuwa kwenye makazi ya binadamu:

1. Kero: Mende huweza kusababisha usumbufu kwa kuzunguka kwenye vyakula na vinywaji.

2. Kuchafua Chakula: Mende hubeba vimelea vya magonjwa wanapopita kwenye chakula.

3. Uoteshaji wa Vimelea vya Magonjwa: Baadhi ya vimelea vya magonjwa huweza kuota ndani ya mfumo wa chakula wa mende.

4. Kuuma: Mende wanaweza kunga'ata na kusababisha majeraha.

5. Aleji: Mate, kinyesi, na mabaki ya mende huweza kusababisha aleji kali.

6. Uharibifu wa Vifaa vya Thamani: Mende huingia kwenye vifaa kama redio na kompyuta, na kuleta uharibifu mkubwa.

Kwa ujumla, ufugaji wa mende unatoa fursa kubwa kiuchumi na kisayansi, na unapoendeshwa kwa ufanisi, unaweza kuwa sekta muhimu nchini.

Jiunge na chanel yetu Unique Hub channel upate taarifa na makala mbalimbali  channel on WhatsApp: https://whatsapp.com/channel/0029VahNCOi4yltWEUtYCD24


0 comments: