Rais Ruto Awaapisha Mawaziri Wapya, Zaidi ya Nusu Wakiwa Mawakili
Rais wa Kenya, William Ruto, leo Alhamisi amewaapisha
mawaziri 19 aliowateua hivi karibuni, huku zaidi ya nusu yao wakitajwa kuwa
mawakili. Kulingana na ripoti za mitandao ya kimataifa, mawaziri wanane kati ya
walioapishwa wanashikilia Shahada za Uzamili na Sheria. Katika orodha hiyo,
Mwanasheria Mkuu mteule, Dorcas Oduor, na Katibu wa Baraza la Mawaziri, Mercy
Wanjau, nao pia ni mawakili, na hivyo kuongeza idadi ya mawakili katika Baraza
jipya la Mawaziri la Rais Ruto kufikia kumi.
Uteuzi wa Rais Ruto unachukuliwa kama hatua ya kukabiliana
na changamoto kadhaa za kisheria ambazo serikali yake imekumbana nazo katika
kipindi cha miaka miwili tangu alipoingia madarakani. Madai haya yamezidi
kuibuka, yakidokeza uwezekano wa ushauri usiofanikiwa wa kisheria kwa Rais na
mawaziri wake.
Miongoni mwa mawakili walioteuliwa ni Waziri wa Mambo ya
Ndani, Profesa Kithure Kindiki, Waziri wa Ardhi, Kazi za Umma, Nyumba na
Maendeleo ya Miji, Alice Wahome, Waziri wa Kawi na Petroli, Opiyo Wandayi,
Waziri wa Elimu, Julius Ogamba, Waziri wa Ulinzi, Roselinda Tuya, Waziri wa
Utalii, Rebecca Miano, Waziri wa Masuala ya Michezo na Vijana, Kipchumba
Murkomen, na Waziri wa Utumishi wa Umma, Justin Muturi.
Katika hotuba yake wakati wa hafla hiyo, Rais Ruto
alisisitiza dhamira yake ya "kutumia kikamilifu fursa zote ndani ya miundo
na mifumo yetu ya kisheria na kitaasisi, ili kushirikiana na asasi za kitaifa
za haki na sheria kwa lengo la kuongeza ufanisi katika uchunguzi wa kesi zote
ndani ya muda uliowekwa."

0 comments: